UONGOZI TULIO NAO NA WANANCHI HAVITANGAMANI- Na Mwalimu Mkuu wa Watu



RAIS WANGU KIKWETE UONGOZI TULIONAO NA WANANCHI HAVITANGAMANI!

Makala Hii imeandikwa Na Pascally Mayega- Mwalimu Mkuu wa Watu

Rais wangu isikie sauti ya mtu aliaye Jangwani ikisema, utukufu uwe
kwa Mungu juu Mbinguni na Duniani iwepo amani kwa watu wenye mapenzi
mema! Viongozi tulionao sasa wanaiona rushwa kama kuwapo kwake ni
sehemu ya mpango wa Mungu.

Hizi ndiyo nyakati za shida zilizotabiriwa
katika maandiko! Taifa lililopoteza maadili huongozwa kwa rushwa,
ambayo nayo huliongoza kuelekea kuzimu!

Rushwa sasa siyo adui tena. Imekuwa ni jambo la kawaida katika maisha
ya kila siku, wala hakuna wakushangaa! Mwenyekiti Taifa wa chama
kinachoiongoza serikali akiwahutubia viongozi wake wa juu alikuwa
mkali. Usoni alionyesha kukerwa na rushwa. Akalikaripia kundi lake
lililokuwa mbele yake. Kwa ukali akawaambia kuwa wakiendekeza rushwa
2015 hawapiti.

Hofu ya Mwenyekiti huyo ni chama na viongozi wenzake kupoteza madaraka
mwaka 2015. Siyo uchungu kwa mateso wanayopata wananchi kutokana na
viongozi kula rushwa. Katika ukali wote ule baba hakuna popote
alipoonyesha kuwahurumia wananchi wake kwa mateso yatokanayo na
rushwa. Anawahurumia viongozi wenzake wa serikali na chama chake.
Wananchi na mateso yao watajua wenyewe! Kwa hili uongozi hautengamani
na wananchi! Tutokako, tuendako hakujulikani!

Ndugu Rais jina la Bwana lihimidiwe kwakuifanya sauti hii isikike kila
pembe ya nchi yetu! Nayo imekuwa faraja kubwa kwa wanyonge na maskini.
Basi na iifikie kila kaya ikawape matumaini mapya wale waliokata
tamaa! Ikawape heshima wale waliodharauliwa! Ikawafariji na kuwapa ari
mpya madaktari, walimu na watumishi wote wengine wenye mioyo
iliyopondekapondeka kwa kulipwa mishahara dhalili na mafao yasiyokidhi
haja ili wengine walipwe kiasi cha kukufuru!

Sauti hii ikawatie shime wamachinga na waponda kokoto na wote
washindao juani! Wanuka jasho na walala hoi nao masela wa maskani,
mama ntilie wa vijiweni wakiisikia sauti hii wapate ufahamu kuwa haya
yote yana mwisho!

Sauti hii ikawatayarishie mwisho mwema na mkamilifu
wazee wote wastaafu wanaopukutika mmoja baada ya mwingine kwa umaskini
wao baada ya kudhulumiwa mafao yao huku waliotakiwa kuwalipa
wakijilipa chekwachekwa! Vijana wa nchi hii waliosoma na wasio soma
wamejaa katika mitaa ya miji yetu wote wakiwa hawana kazi! Masikini
hawa hawaijui kesho yao! Mjinga peke ndiye halioni bomu hili! Sauti
hii ikawe kwao kipoozeo japo cha kupita! Haitashangaza kesho wenye
mamlaka wakiwaita ni wahamiaji haramu! Msaada wao wanawema hawa
utatoka wapi?!!

Mwanamwema Nasoro Mohamed ameifikisha sauti hii hadi gerezani. Wapofu,
badala ya kuisikiliza sauti yake walimtia kifungoni wakidhani
wanamwadhibu. Hawakujua kuwa sasa wanamfua! Nasoro ukiwa gerezani
tambua kuwa hakuna ambacho hakikuandikwa katika kitabu cha Mwalimu
Mkuu wa watu.

Yanatokea ili maandiko yapate kutimia. Elewa hakuna
makali yasiyokuwa na ncha. Ukurasa wa 43 Mwalimu mkuu anasema,
“Mwenyezi Mungu ni mwema, akikupa chakula kigumu hukupa pia na meno
magumu. Eleweni kuwa njia ya ushindi ni ndefu na ngumu, lakini jipeni
moyo kwa maana siku ya ushindi iko karibu. Usiku mzito ni pale karibu
na kucha.”

Rais wangu kila nikiinua macho yangu juu kuutazama mwaka 2015, macho
yangu hupata giza mapema na masikio yangu hufa ganzi kwa kughasiwa na
sauti kali mfano wa nyende ipigwayo na nyenje! Nautazama kwa woga
mwaka 2015 na niuwazapo mawazoni mwangu mwili hunisisimka na wasiwasi
hunijaa katika kifua changu! Maisha baada ya 2015 yamefanana na maisha
ya baada ya kifo! Mtu huyaona katika imani tu!

Salehe mwema husema hatanyamaza nami pia nasema sitanyamaza! Kama
Kristu alivyoulilia mji wa Yerusalem ndivyo hivyohivyo nami naililia
nchi yangu! Nchi yangu kwanza! Wakubwa hawatengamani na wananchi
sababu ya mali. Msaada wetu utatoka wapi?

Wanawema wa nchi hii hakuna wakuwakomboa lazima mjikomboe nyinyi
wenyewe! Laana iliingia katika nchi hii baada ya shetani kuwaingia
baadhi ya viongozi wetu nao kwa ulafi wao wakala tunda kwakulifuta
Azimio la Arusha! Azimio la Arusha lilikuwa ni silaha njema ya
wanyonge na maskini wa nchi hii iliyowalinda wasidhulumiwe na baadhi
ya viongozi wenye makoromeo yenye uchu wa vyote mali nyingi na
madaraka. Wamelifuta na sasa wanaogelea katika pepo ya dunia ya mali
nyingi! Laiti kama ningelikuwa na uwezo wa kumlaani mtu, ningewalaani
watu hawa!

Rais wangu tuliokuwa zamani tulimfahamu Mwene, au Chifu au Mtemi kama
mfano wa mtu mwema, mkarimu aliyewajali wananchi wake katika nchi
yake. Ikulu palikuwa ndiyo kimbilio la maskini. Aliyekosa chakula
alienda kula Ikulu. Kila Ikulu ilikuwa na mashamba makubwa ya chakula
yaliyolimwa na wananchi wenyewe kwa ajili ya yeyote atakayekosa
chakula. Huo ulikuwa wakati wa mila na desturi.

Wakati wa maadili! Leo
maadili yako wapi? Yamekwishakwenda! Kiongozi wa nchi ndiyo anakuwa
kiongozi wa kupora nchi na wananchi wake! Tumeona viongozi kama Mobutu
Sesseseko waliojilipa kupindukia, wakajikusanyia utajiri mwingi
kushinda nchi zao! Lakini leo wako wapi? Wamekwishapita. Nasisi
tunapita!

Rais wangu ya nini kuisumbukia dunia na mambo yake yapitayo? Waziri
mzima bila soni kalifahamisha Taifa kupitia Bunge kuwa kama ikibidi
wafanyabiashara haramu ya madawa ya kulevya kutajwa basi wote
watakwisha! Serikali haijawahi kukanusha neno hili wala Bunge
halijawahi kulikataa! Hata na wabunge ambao wanajiona hawahusiki
hatujawasikia wakimwadabisha. Swala zima limeachwa lionekane kuwa
kweli!

Wananchi wamesikia viongozi wamo katika biashara haramu ya nyara za
serikali. Wameambiwa viongozi wamo kwenye uvunaji haramu wa misitu.
Kutorosha wanyama hai, madini na raslimali nyingi nyinginezo viongozi
wamo. Fedha haramu na mitandao ya kijasusi hakuna mwenye ushahidi kama
hawamo. Kwa watawala aina hii, nani atakuwa tayari kuwarudishia
wananchi ukombozi wao, Azimio la Arusha?

Azimio la Arusha, limewafananisha viongozi wote. Hata uimbeje, si
wanaotawala wala si viongozi wa Upinzani wote hawako tayari kulipatia
nafasi Azimio la Arusha! Uongozi wa nchi ukioza nani anajali?

Azimio la Arusha linapolinda wananchi na kuzuia raslimali za nchi
zisiporwe pia linawazuia viongozi wachache waroho  wa vyote mali na
madaraka wasiwe sehemu ya waporaji wakuu. Haijalishi viongozi hawa
wako madarakani au katika upinzani. Hivyo haishangazi viongozi wa
upinzani nao kulinyamazia Azimio la Arusha! Nao ni wanadamu wenye
shida, maumbile na matamanio yaleyale! Wakumkomboa mwananchi masikini
hapa nani?

Rais wangu wakati wananchi wangali wanalililia Azimio la Arusha kwa
ajili ya ustawi wao na ustawi wa nchi yao huku wakiomba dua ICC idumu
kwa usalama wa maisha yao, Ana Makinda Spika wa Bunge ameonyesha kuwa
kati ya viongozi wasioweza kusoma alama za nyakati. Huu haukuwa wakati
kwake kulilia unono zaidi wa mishahara ya viongozi ambao tayari
umewapalia wananchi.

Ujumbe wa mwanamwema Dosa si uhariri, “P. Mayega shikamoo! Sasa ndiyo
napata picha kwanini Muumba alianza kumuumba baba halafu baada ya muda
kupita akamuumba mama. Hivi kweli Wabunge hawa wenye muda usio na
kikomo eti wakistaafu wanabaki masikini! Kaa, kweli cheo hakiongezi
akili, hekima wala uadilifu. Na Bibi Titi Mohamed nae angewasemeaje
wabunge wa enzi zile za uadilifu na uchapa kazi wa kweli? Ee, Mungu
nakuomba uinusuru nchi yangu Tanzania.

“Hivi ni wabunge gani anaowasemea huyu mama? Ni hawahawa wanaokesha
tangu mwanzo wa kampeni hadi uchaguzi, usiku na mchana, nyumba hadi
nyumba wakigawa vitu na pesa? Eti ni masikini! Mama yangu tema mate
chini na umwogope Muumba wako we mama Makinda. Hivi ndo mmetudharau
kiasi hiki? Baba mwambie mh. Spika tumechoka na tumeishiwa kabisa
uvumilivu juu yao! Au sababu na yeye ni mbunge. Mikate yao ni mikubwa
kuliko ya wahisani wetu. Eti na bado!”

Makinda amesema wakati mbaya. Aliposema tozo ya simu ya sh. 1000 ni
ndogo hata masikini anaweza kulipa yaelekea hakujua alichokuwa
anasema. Sasa baada ya ukubwa wa mishahara yao kujulikana tafsiri ni
kwamba anajenga hoja ili serikali izidi kuwakamua wananchi hata kama
ni kuwakamua damu, lakini pesa lazima zipatikane wabunge waongezewe
mishahara zaidi. Bila Azimio la Arusha wananchi wamekwisha maana kila
kiongozi anakula kulingana na urefu wa makucha yake!

Anachofanya Makinda ni kuzidisha chuki kati ya Bunge na wananchi na
kati ya wananchi na serikali. Wapinzani wanapotetea tozo ya simu
Bungeni, hata kama utetezi wao hautoki katika mioyo yao, mbele ya
wananchi wanaonekana ni watu wa Mungu. Hao wengine wananchi wanawaona
ni mchanganyiko wa kunguru na manyang’au!

Rais wangu tungekuwa na Azimio la Arusha hakuna kiongozi wetu hata
mmoja ambaye angeweweseka anaposikia Mahakama ya uhalifu wa kivita ICC
iliyoko The Heaque nchini Uholanzi inapotajwa. Kwa viongozi wengi ICC
kwao ni sawa na zimwi mla watu ambalo kila walionapo usiku katika
ndoto zao hushtuka na kujikuta wamewanyanyapaa wenzi wao kwa muda! ICC
imeuharibu kwa kiasi kikubwa utamu wa urais, hasa urais wa nchi za
kiafrika.

Rais wangu sijui ni kigezo gani viongozi wa Afrika wanakitumia kulaani
shambulio la Westgate lililotokea jijini Nairobi nchini Kenya. Kwa
ushuhuda unaoendelea kutolewa katika mahakama ya Uhalifu wa Kivita ICC
dhidi ya watuhumiwa, ikiwa mahakama itathibitisha kuwa ni wakweli
utaitisha Dunia kuliko Westgate!

Binadamu wa kweli mwenye kuamini
katika uwepo wa Mungu hawezi kumaliza kusimulia uhalifu unaodaiwa
kufanywa na watuhumiwa bila kuulowesha mwili wake kwa machozi!
Inashindikana kuingia akilini ni kwa kiasi gani binadamu anaweza kuwa
katili kwa binadamu mwenzake! Inaumiza zaidi kujua kuwa wahanga
walikuwa ni watu ambao hawakuwa na hatia yoyote! Waathirika wakubwa
walikuwa wanawake na watoto! Walikosa nini?

Ndugu Rais uhalifu wa Westgate unaonekana kutisha zaidi kwasababu tu
umeongezewa neno moja zaidi ‘ugaidi’, lakini kiuhalifu haufikii hata
robo ya ule uhalifu uliofanywa katika machafuko ya baada ya uchaguzi
wa 2007/2008 nchini Kenya.

Wakenya watatu wameshtakiwa ICC kwa kupanga na kufadhili machafuko ya
baada ya uchaguzi ambapo watu wasiokuwa na hatia wakiwemo akina mama
na watoto walipigwa risasi huku wengine wakikatwakatwa hadi kufa na
magenge ya uhalifu! Ushahidi unaotolewa kutoka ICC unaonyesha jinsi
mamia ya wakenya walivyouawa kinyama baada ya kukimbilia kwenye nyumba
za Ibada kuokoa maisha yao lakini wakajikuta wanamwagiwa mapipa ya
petroli iliyonunuliwa na wafadhili na kisha kuchomwa moto
uliowateketeza wote na nyumba hizo za Ibada hadi kubaki majivu! Unyama
gani huu jamani!

Marais wa kiafrika wanaokumbatia unyama huu
hawatufai! Kwanini wasiache mahakama ithibitishe kama ni kweli? Ni
mwenye roho ya kinyama tu ndiyo anaweza kutetea unyama huu!
Mwanamwema Nyambari alinitumia ujumbe akasema, “Mayega, Mungu
alikujalia hekima na busara.

Tatizo unaowaandikia wamejifanya hamnazo.
Kama vurugu za Kenya ziligharimu takribani roho za Wakenya zaidi 1,200
ni vipi viongozi wetu wanaona huruma sana kwa watu wanaoshtakiwa tu?
Hawa ina maana hawana uchungu kuhusu mauaji yale ya kinyama? Kumbe
ukiua halafu ukagombea urais kesi inakwisha! Hii ni aibu kubwa kwa
bara hili! Na ni aibu kubwa zaidi kwa viongozi wetu! Mbona hawatuambii
ni rais gani wa Afrika ambaye ameshtakiwa bila kufanya kosa! Hawa
wanajiandalia kinga tu halafu waendeshe mauaji na mateso dhidi ya raia
katika nchi zao!”

Mwingine akasema, “Mwalimu, marais wa Afrika wanaoigwaya ICC
wameparaganyika kichwani.  Wanasema mbona wazungu hawakamatwi! Hivi
mwizi wa Iringa asipokamatwa inampa leseni mwizi wa Morogoro
asikamatwe?”

Rais wangu liwalo na liwe lisituchanganye tukajikuta tumejiingiza
kwenye orodha ya marais wa aibu! ICC haitengenezi watuhumiwa. Kama
tunayo sifa, tutafika Uholanzi. Unyama wa kutisha uliotendwa nchini
mwetu katika kipindi hiki hauwezi kupita bure. Wananchi wetu wasio na
hatia wameuawa! Wengine wamefanyiwa unyama mkubwa na wengine wengi
hivi sasa wanaishi kwa hofu! Watuhumiwa wa matukio haya ya kinyama
hawajulikani na mimi sijaja hapa kumuonyesha mtu kidole

Rais wangu umesema wahalifu hao huwajui! Waziri Mkuu amesema hawajui!
Na mimi nasema siwajui! Lakini Mwenyezi Mungu anawajua! Na hukumu yake
ilianza siku na saa ileile ya tukio. Nafsi zao zilianza  kuwasuta na
zitawasuta mpaka siku yao ya kusimama mbele ya haki! Mahakama ya ICC
inahukumu mwili.

Iwepo au isiwepo hukumu ya Mungu ipo palepale!
Baba, uhalifu ukitokea wakwanza kutuhumiwa ni yule aliyekabidhiwa
dhamana ya kuhakikisha uhalifu hautokei. Na aliyekuwa na jukumu la
kuwakamata wahalifu wa uhalifu huo, asipowakamata anakuwa mtuhumiwa
namba mbili . Katika mazingira kama haya tutaikwepa vipi ICC?
https://mail.google.com/mail/images/cleardot.gif

0 comments:

Post a Comment